Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais

Tume ya Utumishi wa Umma

HAKI NA WAJIBU KATIKA UTUMISHI WA UMMA

  Wajibu ni kile ambacho mtu analazimika, anapaswa au hana hiari kufanya; wajibu ni kuhusika juu ya jambo fulani.  Jambo lenyewe lazima liwe linahitaji utendaji, utekelezaji au utimizaji.

Kwa Watumishi wa Umma, wajibu wao, kwa mfano, ni kutoa huduma kwa wananchi mbalimbali katika maeneo na ngazi tofauti tofauti, kuheshimu sheria, kuzingatia maelekezo na maagizo na kutekeleza kazi zote za Mwajiri wake.

Aidha, kwa watumishi wa umma wenye dhamana, wajibu wao ni kuhakikisha kuwa huduma zinatolewa kwa usahihi; kwa wakati na kwa ukamilifu; kuhakikisha kuwa watumishi wana sifa, uwezo na nyenzo na mazingira mazuri yakuwawezesha kutoa huduma, na kuhakikisha kuwa kila mtumishi aliye chini yake amegawiwa majukumu au kazi  na kwamba kila mtumishi anatekeleza majukumu yake ipasavyo.

Kadhalika kuhakikisha haki, maslahi na stahili za watumishi zinatimizwa. Wajibu wakati fulani hufanana kidogo na majukumu katika tafsiri. Wakati mwingine wajibu usipotekelezwa huweza kusababisha mgogoro na mgongano kati ya mwenye wajibu na mtoa haki.

1:1 HAKI ZA MTUMISHI

Haki ni jambo au kitu ambacho mtu anapaswa apate kutoka kwa mtu mwingine au kutoka kwenye mamlaka fulani; inaweza  kuwa  miongoni  mwa  yale  yaliyotajwa kwenye Katiba, Sheria, Kanuni, Maagizo au maelekezo mbalimbali; haki ni lazima kutimizwa au kutolewa na isipotolewa au ikikiukwa hudaiwa.

Wakati mwingine kutotimizwa haki kunaweza kusababisha mgogoro na mgongano kati ya mwenye haki na anayepaswa kuitoa au kuitimiza; na kwa Watumishi wa Umma haki zao ni kama vile maslahi mbalimbali,  mafunzo, kupandishwa cheo, kuheshimiwa, kuthaminiwa, kusikilizwa, kushirikishwa, kurekebishwa na kuadhibiwa.

1:2 WAJIBU WA MTUMISHI WA UMMA

Wajibu wa watumishi wa Umma umejikita katika maeneo manne

a) Wajibu kwa Nchi yake

b)  Kuwa mzalendo na kuipenda nchi yako

c) Kuwa na moyo wa Kujitolea

d)  Utii kwa Serikali iliyopo Madarakani

e) Kuzingatia Sheria za Nchi

f) Kulipa Kodi

1:3 WAJIBU WA MWAJIRI

a) Kufanya kazi kwa bidii – tija na ufanisi kazini

b)  Kutimiza malengo ya kazi

c) Kuzingatia Sheria za Kazi

d)  Kuzingatia Maadili ya Utumishi na Taaluma

1:4 WAJIBU WA WANANCHI / WATEJA TUNAOWAHUDUMIA

a) Kutoa huduma bora kwa ueledi

b)  Kutoa huduma bila upendeleo

c) Kufanya kazi kwa uadilifu

d)  Kutoa maelekezo ambayo ni ya wazi na sahihi


Kurasa za Karibu

Hakimiliki © 2014. Tume ya Utumishi wa Umma. Haki zote zimehifadhiwa.