Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais

Tume ya Utumishi wa Umma

TUME YA UTUMISHI WA UMMA IMEKABIDHIWA KIBALI CHA UJENZI WA OFISI MJI WA SERIKALI MTUMBA

Tume ya Utumishi wa Umma ni miongoni mwa Taasisi za Umma ambazo zimekabidhiwa hati za vibali vya ujenzi wa Ofisi za Taasisi Dodoma.  Katibu wa Tume ya Utumishi wa Umma Bw. Mathew M. Kirama amekabidhiwa hati hiyo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. George B. Simbachawene (Mb) katika hafla iliyofanyika Ukumbi wa Hazina Dodoma.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Waziri Simbachawene (Mb) amesema lengo la hafla hii fupi ya kukabidhi vibali vya ujenzi kwa Taasisi zilizopewa idhini ya ujenzi wa Ofisi Dodoma kama sehemu ya kutambua mchango wa Taasisi hizo katika kuunga mkono utekelezaji wa Mpango wa Serikali kuhamishia shughuli zake Jijini Dodoma hasa kwa kuzingatia kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu ndio yenye wajibu wa uidhinishaji wa vibali vya ujenzi wa Taasisi za Serikali katika Makao Makuu ya Nchi.
Mheshimiwa Simbachawene amesema Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kutekeleza kikamilifu Mpango wa kuhamia Dodoma ambapo Wananchi wanapata huduma zote katika Makao Makuu ya Nchi. Aidha, watumishi wote wa Serikali ikiwemo Wizara zote, Vyombo vya Ulinzi na Usalama na Mhimili wa Bunge na baadhi ya Taasisi wamehamia Dodoma na wanaendelea kutekeleza majukumu yao.
Akizungumzia Sheria ya kuitambua Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi (Capital City Declaration Act of 2018) alisema ilipitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tangu Septemba 2018 na majengo yote ya Wizara na Taasisi za Serikali yanaendelea kujengwa Dodoma badala ya Dar es Salaam.
Majengo haya ya Taasisi  yanajengwa katika maeneo ya NCC link, Medeli, Njedengwa, Mtumba na Kikombo na yanajengwa kwa kufuata Mwongozo uliopo katika Mpango Kabambe wa Jiji la Dodoma ambao Ofisi ya Waziri Mkuu ina jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wake.
Mheshimiwa Simbachawene ametoa taarifa kuwa pamoja na ujenzi wa Ofisi za Taasisi unaoendelea, Serikali imekamilisha ratiba na Mwongozo utakaowezesha Taasisi za Serikali ambazo bado zinaendelea kutekeleza majukumu yake Dar es Salaam kuweza kuhamishia shughuli zao Jijini Dodoma kwa awamu.
"Katika utekelezaji wa suala hili, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo kwamba Taasisi 42 zihamie Dodoma ndani ya mwaka huu wa fedha 2022/2023. Taasisi 36 zitahamia Dodoma katika mwaka ujao wa fedha wa 2023/2024 na Taasisi 19 zitahamia katika mwaka wa fedha 2024/2025 wakati Taasisi 27 zimeelekezwa kwamba kwa kuzingatia aina ya majukumu zilizonazo, kuendelea kutekeleza majukumu yao Mkoani dar es Salaam. Hatua hii itakamilisha sehemu kubwa ya Mpango wa Serikali wa kuhamia Dodoma ambapo hadi sasa tayari Taasisi 65 zilishahamia Dodoma tangu mwaka 2016 hadi 2022".
Mheshimiwa Simbachawene ametoa wito kwa Viongozi wa Mkoa wa dodoma, Wizara, Halmashauri, Taasisi za Serikali, Sekta Binafsi, Wananchi na wadau wengine kuendelea kutoa ushirikiano katika utekelezaji wa Mpango wa Serikali wa kuhamia Dodoma.  

Kurasa za Karibu

Hakimiliki © 2014. Tume ya Utumishi wa Umma. Haki zote zimehifadhiwa.